SIMBA YAWAPINGA NCHUNGA, MADEGA TFF


                                                                           Lloyd Nchunga
Imani Madega
MABINGWA wa Ligi Kuu Bara, Simba ya jijini Dar es Salaam, wamewasilisha barua Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), wakimpinga Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho hilo, Wakili Alex Mgongolwa, pamoja na wajumbe wake wawili kwa madai ya kutokuwa na imani nao.
Wajumbe waliopingwa sambamba na Mgongolwa ni waliowahi kuwa wenyeviti wa klabu ya Yanga, mawakili Lloyd Nchunga na Iman Mahugila Madega.
Pingamizi hilo la Simba, linatokana na kutokuwa na imani na viongozi hao katika kuamua suala la usajili wa wachezaji waliozua utata, Kelvin Yondani na Mbuyu Twite, ambao awali Simba inadai iliwasajili kabla ya Yanga kuingilia kati na kuwanyakua.
Kamati hiyo ilikuwa ikutane jana na leo kwa ajili ya kupitia usajili wa klabu za Ligi Kuu Bara na Ligi Daraja la Kwanza, lakini kutokana na kusogezwa mbele kwa ligi hiyo, wanatarajiwa kukutana katika tarehe itakayopangwa baadaye.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga ‘Mr. Liverpool’ alisema wamewasilisha barua hiyo ili kuomba kushughulikiwa kwa ombi lao kwa hofu ya kutotendewa haki.
Alisema kuwa Mgongolwa pamoja na kuwa mwenyekiti wa kamati hiyo, pia amepata kuwa mjumbe wa kamati za Yanga, huku Madega na Nchunga nao wakiwa ni wanachama waadilifu na waaminifu wa klabu hiyo, hivyo ni rahisi kuipendelea.
Aliongeza kuwa kutokana na wajumbe hao wa kamati kuwa na damu ya Yanga, wanaamini hawatatoa maamuzi sahihi kuhusiana na suala linalohusu utata wa usajili wa wachezaji hao, hivyo TFF haina budi kutumia busara kuwaondoa.
Hivi karibuni, Mwenyekiti wa Simba, Alhaj Ismail Aden Rage, alitangaza kujiuzulu ujumbe wa kamati hiyo, kabla ya Rais wa TFF, Leodegar Tenga, kukutana naye na kumweka sawa, hivyo kubadili msimamo wake.

Post a Comment

Previous Post Next Post