TFF YAFAGILIA UDHAMINI WA VODACOM


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limeishukuru Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom kwa kuingia mkataba mpya wa udhamini wa ligi kuu soka tanzania Bara.
 Rais wa TFF, Leodegar Tenga alisema kuwa, mkataba huo ambao ni mnono na mara mbili zaidi ya ule wa uliopita, anaamini utazisaidia vilivyo klabu shiriki.
“Ni wazi kuwa, mkataba huu una maslahi kwa klabu zetu pamoja na soka la Tanzania kwa ujumla, kwa sababu umeongeza maradufu fedha za udhamini,” alisema Tenga.
Tenga alisema kuwa, kuhusu wadhamini hao kuondoa nembo kifuani na kuweka mabegani, ni hatua nyingine kubwa inayotoa fursa ya kuziwezesha klabu kunufaika.
Alisema, kwa sasa klabu zitaruhusiwa kuweka mabango ya wadhamini wowote watakaowapata, isipokuwa wale ambao ni washindani wa Vodacom kibiashara.
Aidha, Tenga ameishukuru pia SuperSport kwa kukubali mwaka huu kuonesha mechi nyingi zaidi ya mwaka jana na mwaka juzi.
“Hii ni faraja kubwa sana kwetu, kwa sababu mwaka jana na mwaka juzi SuperSport walionesha mechi za Yanga na Simba tu,” alisema Tenga.
Tenga alisema kuwa, hilo litasaidia kulitangaza soka la Tanzania nje ya nchi na kuvuta wawekezaji, pamoja na wadhamini wengi zaidi wa ndani na nje ya nchi.
Aidha, Tenga aliwaomba wadhamini kujitokeza kudhamini timu ya Taifa ya Wanawake, ‘Twiga Stars’ pamoja na zile za vijana chini ya miaka 20, U-20 ‘Ngorongoro Heroes’ na U-17 ‘Serengeti Boys’.
Lakini wakati Tenga akiipongeza Vodacom, timu kadhaa zinazoshiriki ligi kuu bara, zimekuwa zikivutana na Shirikisho hilo kwa madai hazinufaiki ipasavyo kutokana na gharama wanazotumia hivyo kutaka kuruhusiwa kusaka wadhamini wengine ikiwamo washindani kibiashara na Vodacom.
Katika hatua nyingine, pambano kati ya Azam FC na JKT litakalopigwa leo Iwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, litaoneshwa ‘live’ na SuperSport kuanzia saa 1:00 jioni.

Post a Comment

Previous Post Next Post