Mwandishi Wetu
Bonanza kubwa la mchezo wa mpira wa miguu linaloitwa 'Nane
nane soccer bonanza' linatarajiwa kufanyika kwenye viwanja vya Tanganyika
Parkers Kawe jijini Dar es Salaam siku ya kilele cha sherehe za nane nane.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mkurugenzi wa kampuni ya
SULE'S INC. & ENTERTAINMENT, Salum Suleiman ambao ndiyo waandaaji wa
Bonanza hilo timu mbalimbali kutoka katika maeneo ya wilaya ya Kinondoni jijini
Dar es Salaam zitashiriki.
"Maandalizi ya bonanza hili yameshafikia katika hatua
nzuri kabisa, Kamati imefanya kazi nzuri mpaka kufikia hapa na tunategemea
bonanza hili litafanyika kwa mafanikio makubwa,"alisema Suleiman.
Akizungumzia timu zitakazoshiriki katika bonanza hilo,
Suleiman alisema,"tunatarajia kuwa na timu nane ambazo zitachuana katika
kuwania kombe siku hiyo na mashindano yataendeshwa kwa mtindo wa mtoano."
Alisema wameamua kuliendesha bonanza hilo kwa mtindo wa
mtoano ili timu ziweze kutoa ushindani wa kutosha na kuburudisha watu watakaojitokeza
katika bonanza hilo.
"Washindi watapata zawadi, kwa sababu mshindi wa kwanza
atatwaa kombe, mshindi wa pili pia atapata zawadi, mchezaji bora, mfungaji
bora, kipa bora na mchezaji mwenye nidhamu wote hao watapata zawadi."
Sherehe za nane hufanyika kila mwaka sehemu mbalimbali
nchini ikiwa ni siku ya kuadhimisha siku ya wakulima.