Na Dina
Ismail
TANZANIA  ni moja ya  nchi zinazoaminika na kusifika  kuwa  na
 watu wenye amani, upendo na ushirikiano.
Kweli!  tunasifika kwa hilo toka kwa watu wa nje,
lakini kwa kiasi kikubwa hali hiyo haipo baina yetu katika baadhi ya makundi ya
kijamii.
Tukiangalia  katika  sekta 
ya sanaa na  michezo  suala la kutowathamini watu hao lipo na
linaendelea kushika kasi kila kukicha.
Hapa kwetu,msanii
au mchezaji anakuwa  anathaminiwa au
kupendwa pindi  anapokuwa  mzima wa afya 
na mwenye nguvu zake.
Tofauti na
nchi za wenzetu ambazo hata kama zina machafuko lakini wasanii na wanamichezo
wanathaminiwa katika hali zote mradi tu amepata kutoa mchango wa kisanaa na
michezo katika nchi yake.
 Kwamba, kwa Tanzania thamani ya wasanii na
wachezaji  inaonekana pindi wanakuwa
katika uzima na afya njema lakini 
wakipatwa na ugonjwa au umauti hakuna anayejali.
Tumeshuhudia
mara kwa mara taarifa za wasanii na wanamichezo kuomba msaada wa matibabu
wanapopata maradhi lakini mapokeo ya maombi yao huwa si ya kuridhisha.
Matokeo yake
jukumu la kuuguza hubaki kwa wanafamilia na kwa bahati mbaya kuna wanaofikwa na
umauti au kilema kutokana na maradhi yao na hakuna anayejali.
Kama hiyo
haitoshi, kuna baadhi ya wachezaji wamejikuta wakikatiza ndoto zao baada ya
kuumiwa wakizitumikia timu zao na bila huruma wanatelekezwa bila msaada
wowote  kubaki wakijiuguza wenyewe.
Hili
linasikitisha sana, kwani pamoja na mchezaji kuumia akiwa chini ya himaya yako
bado unamuacha akahangaike kujitibia mwenyewe sasa hapo thamani yake iko wapi.
Kwamba,
utaona ufahari kujitokeza katika msiba wake na kutangaza kuwasilisha kiasi
kadhaa cha ubani,hilo hata mungu hapendi kwani kama mlikuwa mnamthamini
mngemuhudumia kuanzia mwanzo mpaka pale ahadi yake itakapofika.
Hebu tuachane
na roho za kikatili kwa watu wetu hawa kwani kwa namna moja ama nyingine
wanasaidia kuitangaza nchi, wanasaidia kukupa wewe kula, wanasaidia kukupa  wewe heshima, wanatoa burudani, wanaelimisha
na mengineyo mengi.
Pamoja na
yote mazuri na michango yao katika jamii lakini hatuwathamini kama
inavyostahili kulingana na waliyoyafanya wakati wa uzima au uhai wao.
Kama hiyo
haitoshi, kuna wengine wanakumbwa na umauti na hata timu, taasisi au kundi
alilokuwa akilifanyia kazi linashindwa hata kuhudhuria katika msiba wake.
Basi
umeshindwa kuhudhuria msiba, mfano mchezaji huyo alipata kuwa tegemeo katika
timu yako na kucheza kwa mafanikio leo anazikwa na timu yako inacheza lakini
unashindwa hata kusimama kwa dakika moja tu kumuombea.
Watanzania
tubadilike kwa kuthamini na kujali wenzetu!

